Monday 20 February 2017

Jumuiya ya Kiisilamu yataka MATEJA Wote washtakiwe na Pia Mali za Paul Makonda Zichunguzwe

Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini imevitaka vyombo vya kisheria na uchunguzi kuacha kupuuza kauli zilizotolewa na wabunge zilizomtuhumu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kumiliki mali zisizoendana na kipato chake halali.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kaimu Msemaji wa Jumuiya hiyo Sheikh Rajabu Katimba, alisema wakati wa mkutano wa Bunge lililopita baadhi ya wabunge walimtuhumu Makonda hivyo tuhuma hizo zinapaswa kufanyiwa kazi kwa mujibu wa sheria.
Alisema vyombo vyenye mamlaka ya uchunguzi vinapaswa kufanya uhakiki wa mali za Makonda ili kuondoa shaka katika umiliki wa mali aliyonayo na uhalali wa misaada ya kifedha zinazotolewa kwake na taasisi rafiki.
Sheikh Katimba alisema kifungu cha (11) cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma inamtaka kiongozi kutaja hadharani mali zake ikiwemo zawadi anazopewa.
Hivi karibuni, Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) wakati akichangia taarifa za Kamati ya Bunge na Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama alisema Makonda amenunua jengo ‘(Apartment ) lenye thamani ya shilingi mil 600 jijini Dar es Salaam.
Selesini aliliambia Bunge kuwa Makonda amempa gari mkewe aina ya Mercedez Benzi lenye thamani ya Dola 250,000 za Marekani ambazo ni sawa na Sh milioni 550.
Mbali na Selesini, Mbunge mwingine aliyemtuhumu Makonda kujilimbikizia mali ni Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Msukuma (CCM) ambaye naye wakati akizungumza bungeni alihoji ni wapi Makonda alipata fedha za kusafiri kwenye ndege daraja la juu kwenda Marekani.
Wakati huo huo, Sheikh Katimba alisema vita dhidi ya dawa za kulevya inaweza kwenda vibaya iwapo itasimamiwa na wanasiasa.
Alisema ili kuepuka hilo vyombo vya dola vyenye mamlaka ya kisheria vinapaswa kuifanya kazi hiyo kwa weledi mkubwa.
Sheikh Katimba alisema taasisi za kiislamu zinaunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali kupambana na biashara hiyo na kusisitiza kuwa vyombo vyenye mamlaka kuisimamia kwa mujibu wa Sheria ya Kudhibiti na Kupambana Dawa za Kulevya nchini ya mwaka 2014.


‘’Hatuoni ni kwa mantiki ipi watumiaji wengine washitakiwe kwa kutumia dawa na wengine waachiwe huku zitumike na fedha za kuwatibia nje ya nchi.

‘’Wasanii kama Rehema Chalamila, maarufu kwa jina la Ray C’ msanii TID nao pia walipaswa kushitakiwa kama walivyofanywa wengine na vilevile watumiaji walioko mitaani na kwenye vituo vya daladala wote wasombwe wakapimwe na kisha washitakiwe.

“Pamoja na nia ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuongoza na kuendesha vita hiyo lakini vita isimamiwe na vyombo vyenye weledi na si wateule wa kisiasa au wanasiasa,’’ alisema.

Aidha, alizungumza kesi za ugaidi inawakabili baadhi ya viongozi wa dini kwa kueleza kuwa haitakuwa na tija wala heshima iwapo viongozi hao wataendelea kushikiliwa gerezani.

“Ni kweli serikali inatutaka tuiunge mkono kwenye vita hiyo nasi tuko tayari lakini ni vuziri jitihada hii ikawa kwa watu wote, tunaiona serikali inashindwa kutenda haki kwa viongozi wa dini yetu na ni kesi gani isiyokwisha? inatia aibu masheikh kufungwa bila hatia miaka mitatu ni sawa na kufungwa bila hatia,’’ alisema Sheikh Katimba.

from Blogger http://ift.tt/2lC8S1v
via IFTTT




from WordPress http://ift.tt/2kZacYJ

No comments:

Post a Comment